Jumatatu, 27 Shawwal 1445 | 2024/05/06
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

Afisi ya Habari
Wilayah Iraq

H.  28 Dhu al-Hijjah 1444 Na: 1444 / 19
M.  Jumapili, 16 Julai 2023

Taarifa kwa Vyombo vya Habari

[يُرِيدُونَ لِيُطْفِؤُوا نُورَ اللهِ بِأَفْوَاهِهِمْ وَاللهُ مُتِمُّ نُورِهِ وَلَوْ كَرِهَ الْكَافِرُونَ]
“Wanataka kuizima nuru ya Mwenyezi Mungu kwa vinywa vyao. Na Mwenyezi Mungu atakamilisha nuru yake ijapo kuwa makafiri watachukia.” [As-Saff:8]
(Imetafsiriwa)

Tangu kukaliwa kimabavu kwa Iraq mwaka 2003, mvamizi Marekani imekuwa ikicheza karata ya kimadhehebu na hata kuanzisha mfumo wa kimadhehebu na kikabila ili kuisambaratisha nchi hiyo. Waliamua kugawanya sehemu za Masunni na Waarabu kutoka kwa Wakurdi na kutangaza kwamba sehemu ya Mashiya inawakilisha idadi ya walio wengi. Kwa hiyo, waliamini kuwa ilikuwa ni haki yao kuunda na kuongoza serikali, wakiwaleta vibaraka wao wenyewe na kuwaweka juu ya vichwa vya watu wa Iraq. Waliuachia utawala wa Iran kuwa chombo chao katika kutekeleza mpango huu muovu, wakianza na wanasiasa waliowateua, wakijua kikamilifu uaminifu wao kamili kwa utawala wa Iran. Hii ilifuatiwa na kuundwa kwa makundi yenye silaha, ambayo mengi yalichaguliwa kwa mkono, na yakawa nguvu na mamlaka juu ya serikali iliyowakilishwa na jeshi. Yalitoa huduma muhimu katika kutekeleza mpango wao nchini Iraq na Syria, na mizozo ya vyombo vya habari kati yao na utawala wa Iran na wafuasi wake haikuwa chochote ila wingu la moshi la kupofusha macho ya watu wa Iraq.

Mvamizi huyo wa Kimarekani, pamoja na zana zake zilizowakilishwa na Iran na makundi yenye silaha, walifanikiwa kuisambaratisha nchi hii, na kuwatumbukiza watu wake katika giza tororo na kuzusha mizozo. Watu wa Iraq walilipia gharama kubwa katika suala la umwagikaji damu, kuhama na kufungwa jela. Iran ilifanya kazi kuifanya Iraq kuwa kina chake cha kimkakati na imesema wazi mara kadhaa kwamba inadhibiti Iraq. Baadhi ya maafisa wake hata wameeleza kuwa Baghdad iko chini ya utawala wa Tehran, na ukweli unathibitisha hilo. Kila mtu anafahamu kiwango cha ushawishi unaotolewa na baadhi ya viongozi wa kisiasa na kijeshi wa Iran kupitia ziara zao za mara kwa mara nchini Iraq na mikutano ya faragha katika kuunda serikali mtawalia.

Mvamizi wa Kimarekani hakusahau kile upinzani ulichokifanya ili kuwafedhehesha na kuzisukuma pua zao kwenye uchafu. Ilikuwa ukingoni mwa kuondolewa lau si kwa ajili ya uokozi wa Iran na kuelekezwa upya kwa silaha za upinzani kuelekea kwenye machafuko ya upofu wa kimadhehebu, yaliyochochewa na vibaraka wao wenyewe. Hili lilifanywa ili kuwafanya watu wa nchi hiyo wajishughulishe na kuuwana wao kwa wao na kumwaga damu zao, badala ya kuungana kama mkono mmoja dhidi ya kafiri anayeikalia kwa mabavu, washirika wake na vibaraka wake.

Kila wakati watu hawa walioshindwa wanapojaribu kuponya majeraha yake na kuamka kutoka katika usingizi wake, mtu muovu wa kimadhehebu hujitokeza kueneza sumu na kutonesha tena majeraha yake. Mfano wa hivi punde ni kauli iliyotolewa na Waziri Mkuu wa zamani na kiongozi wa Chama cha Dawa, Nouri al-Maliki, wakati wa sherehe iliyoandaliwa na Chama cha Dawa katika kile kinachoitwa Siku ya Ghadir mnamo Julai 8, 2023. Alidai kuwa maswahaba, kwa muda wa miaka 70, walikuwa wakimlaani na kumtukana Ali, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, wakati wa sherehe ya Idd. Hakuridhika na hilo, alimtaja Amr ibn al-Aas kuwa muovu na Abu Musa al-Ashari kama msaliti, akilenga kujishindia jamii ya Mashia wasio na habari na kujikusanyia uungwaji mkono katika uchaguzi ujao wa baraza la majimbo uliopangwa kufanyika mwishoni mwa mwaka huu. Hili pia ni jaribio la kuziba mgawanyiko uliotokea ndani ya kipengele hiki kutokana na mamlaka na misimamo ya kisiasa wakati wa kuundwa kwa serikali, hasa na wafuasi wa vuguvugu la Sadr.

Walakini, hali zinaweza kubadilika bila kutarajia. Mnamo siku ya Jumapili, Julai 16, 2023, wafuasi wa vuguvugu la Sadr walichukua hatua kwa kufunga afisi zenye uhusiano na Chama cha Dawa katika eneo la kati na kusini mwa Iraq, kama kulaani dhidi ya kile walichokiona kama "matusi" yaliyoelekezwa na chama kwa kiongozi wao wa kidini aliyefariki, Ayatollah Mkuu Mohammed Mohammad Sadiq al-Sadr. Hili lilimfanya al-Maliki kuwa na wasiwasi, na akatoa taarifa iliyobebwa na Shafaq News, akionya juu ya hatari ya ugomvi wa kipofu katika awamu hii muhimu wakati watu wetu wanatarajia kwa hamu usalama na utulivu wa nchi, baada ya kuchoshwa na mizozo na migogoro. Amesisitiza kuwa, kuwagawanya watu na kuzusha uhasama baina ya mirengo tofauti kunatumikia maslahi ya maadui wanaotaka kuhujumu nguvu zote zenye ufanisi na wema katika jamii. Taarifa hiyo pia imelitaka Baraza la Wawakilishi kutunga sheria inayokataza madhara yoyote kwa viongozi wa kidini walio hai na waliokufa kwa mujibu wa katiba. Ilionyesha matumaini kwamba kambi zote za bunge zingeunga mkono mbinu hii ya kutunga sheria katika baraza hilo.

Enyi Waislamu wa Iraq, kikombe kimejaa na mafuriko yamefika kileleni. Kulia na kuomboleza hakutakuleteeni faida maadamu mnaishi katika udhalilifu, unyonywaji, ghiliba, mauaji, uhamisho, ufisadi, wizi, huduma duni, na mabadiliko ya idadi ya watu katika maeneo na miji mingi. Mzunguko utaendelea isipokuwa murudi kwenye haki na kutii amri ya Mola wenu kwa kufanya kazi ya kusimamisha sheria yake. Wakati umefika wa nyinyi kustahamili haya yote tena na kusimama pamoja kama kitu kimoja, katika mapinduzi makubwa yanayovunja ngome ya shetani. Chuki yao imedhihirika vinywani mwao, na wanayoyaficha nyoyoni mwao ni makubwa zaidi. Naapa kwa Mwenyezi Mungu mambo ya Umma huu hayatarekebishwa isipokuwa kwa yale yaliyorekebisha mwanzo wake, na ni kipi kilichorekebisha mwanzo wake isipokuwa Uislamu?! Tunakuombeni enyi Waislamu kwa ajili ya heshima ya dunia na Akhera fanyeni kazi ya kuregesha mfumo kamili wa maisha ya Kiislamu kupitia kusimamisha Khilafah Rashida kwa njia ya Utume.

[يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ اسْتَجِيبُواْ لِلّهِ وَلِلرَّسُولِ إِذَا دَعَاكُم لِمَا يُحْيِيكُمْ وَاعْلَمُواْ أَنَّ اللهَ يَحُولُ بَيْنَ الْمَرْءِ وَقَلْبِهِ وَأَنَّهُ إِلَيْهِ تُحْشَرُونَ]

“Enyi mlio amini! Muitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume anapo kuitieni jambo la kukupeni uzima wa milele. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu huingia kati ya mtu na moyo wake, na kwamba hakika kwake Yeye tu mtakusanywa.” [Al-Anfal:24]

Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir
katika Wilayah Iraq

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Wilayah Iraq
Address & Website
Tel: 

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu