Ijumaa, 09 Dhu al-Qi'dah 1445 | 2024/05/17
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Ukatili Dhidi ya Wanawake Kamwe Hautatatuliwa Chini ya Mfumo Wowote wa Kiliberali

(Imetafsiriwa)

Habari:

Mnamo tarehe 2 Julai, mamia ya watu walijiunga na mkesha wa Zara Aleena ambaye aliuawa akiwa njiani kuelekea nyumbani kwake Ilford, London Mashariki. Mwanafunzi huyo wa sheria mwenye umri wa miaka 35 alikuwa dakika chache tu kutoka kwenye mlango wake wa mbele alipoburutwa, kupigwa mateke na kukanyagwa na mtu asiyemfahamu. Alipata majeraha mengi mabaya na alionekana akivuja damu na akijitahidi kupumua. Mauaji yake yanasimama pamoja na mauaji mengine makubwa ya wanawake vijana nchini, kama vile Sarah Everard na Sabina Nessa, na kwa mara nyingine tena yameibua mjadala wa kitaifa kuhusu kiwango cha 'janga' la ukatili unaoathiri wanawake nchini Uingereza.

Maoni:

Kwa mujibu wa Afisi ya Takwimu za Kitaifa (ONS), kati ya Aprili 2020 na Machi 2021, wanawake 177 waliuawa nchini Uingereza na Wales pekee, 92% kati yao waliuawa na wanaume. Huu sio uhalifu unaofanywa na wageni peke yao. Badala yake kulingana na ONS, 60% ya wanawake waliouawa nchini Uingereza na Wales walimjua mshukiwa wao wa mauaji na theluthi moja ya washukiwa walikuwa wapenzi wao wa sasa au wa zamani au mume. Kwa kweli, nchini Uingereza, wanawake wawili wanauawa kila wiki na mpenzi wa sasa au wa zamani (ONS). Zaidi ya hayo, huu ni uhalifu ambapo wahasiriwa pamoja na wahalifu wanatoka katika nyanja zote za maisha. Mtu aliyemuua Sarah Everard kwa mfano alikuwa afisa wa polisi anayehudumu.

Mikesha ya kuwakumbuka wanawake vijana na wasichana waliouawa wakitembea katika barabara za Uingereza imeanza kuwa jambo la kawaida nchini humo. Hata hivyo, Uingereza haiko peke yake katika kiwango cha kutisha cha mauaji ya wanawake na ukatili dhidi ya wanawake. Uhalifu huu umekithiri ndani ya dola zengine huria kutoka mashariki hadi magharibi. Nchini Ufaransa, mwanamke mmoja huuawa kila baada ya siku tatu na mpenzi au mpenzi wa zamani, huku unyanyasaji wa kindoa huathiri wanawake 220,000 wa Kifaransa kila mwaka (The Guardian, 2019). Nchini Marekani, karibu wanawake watatu wanauawa kila siku na unyanyasaji wa kinyumbani (Afisi ya Haki) na mmoja kati ya wanawake watano wamebakwa katika maisha yao (Kituo cha Kudhibiti na Kukinga Magonjwa).  Nchini Australia, mwanamke mmoja hulazwa hospitalini kila baada ya masaa matatu kutokana na unyanyasaji wa kinyumbani (Taasisi ya Afya na Ustawi ya Australia). Na nchini Uturuki, wanawake wanne kati ya kumi nchini humo wanakabiliwa na unyanyasaji wa kinyumbani (Taasisi ya Takwimu ya Uturuki), na kwa mujibu wa Wizara ya Sheria ya Uturuki, kuanzia 2003-2014, kulikuwa na ongezeko la 1,400% la mauaji ya wanawake.

Mauaji ya Zara Aleena kwa mara nyengine tena yameibua mjadala juu ya kwa nini wanawake wengi wanafanyiwa ukatili na wanaume ndani ya Uingereza na kushindwa kabisa kwa serikali mtawalia kushughulikia suala hilo. Ni wazi kwamba dhana ya ‘Usawa wa kijinsia’, inayotetewa na wengi ndani ya dola za kiliberali za kisekula kama njia ya kuasisi heshima kwa wanawake, imeshindwa kutoa usalama wa kimsingi kwa wanawake. Uingereza kwa mfano ni mmoja wa watiaji saini CEDAW na Mkataba wa Istanbul juu ya Unyanyasaji dhidi ya Wanawake; ni sehemu ya Mkakati wa Ushirikiano wa Usawa wa Jinsia wa Tume ya Ulaya; ina idadi ya vifungu vya sheria za usawa wa kijinsia zilizotiwa saini kuwa sheria za kinyumbani, kama vile Sheria ya Usawa 2006 na 2010, na Sheria ya Ubaguzi wa Jinsia ya 1975 na 2002; ina Waziri wa Wanawake na Usawa na Kamati ya Wanawake na Usawa. Vitendo na mikataba kama hiyo imejumuishwa katika sheria na katiba ndani ya dola zengine huria, lakini wameshindwa hata kupunguza ukubwa wa unyanyasaji dhidi ya wanawake katika nchi hizi. Zaidi ya hayo, dola kama vile Uturuki na Tunisia ambazo ni viongozi katika kutetea na kutabikisha sera na sheria za usawa wa kijinsia katika ulimwengu wa Kiislamu, pia ni miongoni mwa viongozi wa dunia katika unyanyasaji dhidi ya wanawake.

Ni wazi kwamba kuweka usawa wa kijinsia katika dori na haki za familia, au ndani ya mahali pa kazi au hata ndani ya siasa sio kichocheo cha kujenga heshima na usalama kwa wanawake ndani ya jamii. Badala yake, kufikia matokeo haya kunategemea mtazamo ambao wanaume wanao juu ya wanawake na nyanja zengine za kijamii ndani ya jamii. Ndani ya dola za kisekula, uhuru huria wa kibinafsi na wa kijinsia ambao unawahimiza wanaume kuwatazama na kuwatendea wanawake kulingana na hawaa na matamanio yao, pamoja na kuwashusha thamani wanawake kiutaratibu kupitia kuwafanya kuwa ni vyombo vya ngono katika burudani, utangazaji, ponografia na tasnia zengine pamoja na maisha ya ufuska yaliyokithiri pombe na madawa ya kulevya wameunda mfinyango hatari kuhusiana na usalama wa wanawake. Fauka ya hayo, kukosekana kwa dori, majukumu na haki ya jinsia katika maisha ya ndoa na familia chini ya mifumo ya kiliberali ya kisekula ni kichocheo cha maafa kwa sababu kunaleta mkanganyiko, ushindani na mvutano juu ya wajibu na stahili ambazo huzidisha badala ya kupunguza unyanyasaji wa kinyumbani.

Uislamu kinyume chake una mkabala uliofafanuliwa wa ngazi mbalimbali wa kuzuia na kukabiliana na unyanyasaji dhidi ya wanawake. Kwanza, unakataa uhuru huria wa kijinsia na wa kibinafsi na badala yake unakuza dhana ya Taqwa (Ucha Mungu) ndani ya watu binafsi ambayo inakuza fikra ya uwajibikaji na majukumu katika jinsi wanaume wanavyo watazama au kuamiliana na wanawake katika maisha ya faragha au ya umma. Pili, dalili za Kiislamu zinawalazimu wanaume kuwatazama na kuamiliana na wanawake kwa heshima na kulinda utu na ustawi wao daima. Mwenyezi Mungu (swt) asema: “Enyi mlio amini! Si halali kwenu kuwarithi wanawake kwa nguvu. Wala msiwadhikishe...” [An-Nisa: 19]. Tatu, Uislamu unakataza waziwazi aina yoyote ya dhulma au unyanyasaji wa wanawake. Mwenyezi Mungu (swt) asema: (وَلَا تُضَارُّوهُنَّ  لِتُضَيِّقُوا عَلَيْهِنَّ)  “wala msiwaletee madhara kwa kuwadhiki.” [Al-Talaq: 6] Na Mtume (saw) amesema: ‏ «لاَ تَضْرِبُوا إِمَاءَ اللَّهِ »‏‏ “Msiwapige watumishi wa kike wa Mwenyezi Mungu(Sunan ibn Majah). Nne, Uislamu unaharamisha kuwafanya wanawake kuwa vyombo vya ngono, au kitendo chochote kinachodhalilisha hadhi yao katika jamii, ikiwemo kuwashughulisha na kazi au huduma yoyote inayoitumia miili yao au urembo wao kwa ajili ya faida. Tano, Uislamu unaharamisha dawa za kulevya, pombe na aina yoyote ya maisha ya ufuska ambayo huchangia unyanyasaji dhidi ya wanawake. Na hatimaye, Uislamu unapangilia wajibu na haki za wanaume na wanawake ndani ya ndoa na maisha ya kifamilia kwa njia ya kina na inayosaidiana - kwa mfano kumfafanua mwanamume kama mlezi na mtoa matumizi wa familia na mwanamke kama mjenzi wa nyumba na mlezi mkuu wa watoto. Hii inahakikisha haki na mahitaji ya wanafamilia wote yanatimizwa, na kujenga maelewano na kupunguza mizozo na migogoro juu ya majukumu ambayo inaweza kuzidisha unyanyasaji wa kinyumbani. Pindi kanuni na sheria kama hizi zinapotabikishwa katika ngazi ya dola na nidhamu ya kisiasa ya Uislamu - Khilafah kwa njia ya Utume, hujenga jamii ambayo kwayo wanawake hujihisi kuheshimiwa na salama ndani ya nyumba zao, mabarabarani na maisha ya umma kwa jumla.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Dkt. Nazreen Nawaz
Mkurugenzi wa Kitengo cha Wanawake katika Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu