Jumatatu, 12 Dhu al-Qi'dah 1445 | 2024/05/20
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

Watu walio katika Utumwa wa Kiakili Hawana Haki ya Kuongoza Majeshi ya Waislamu

(Imetafsiriwa)

Habari:

Akizungumza kama mgeni rasmi katika mjadala ulioandaliwa na Taasisi ya Kimataifa ya Mafunzo ya Kimkakati ya Bangladesh (BIISS) kuhusu diplomasia ya ulinzi, Mkuu wa Majeshi wa Jeshi la Bangladesh SM Shafiuddin Ahmed alisema, ‘Sisi ni marafiki kwa wote, lakini kumfanya rafiki mmoja kuwa na furaha, hatuwezi kuwachukiza wengine. Mtu anaweza kuwa rafiki leo, lakini nini kitatokea ikiwa hawatakuwa marafiki kesho?’ Alisema nia ya nchi inaweza kubadilika mara moja, lakini si uwezo wake. Bangladesh ilihakikisha uwiano kati ya Marekani na China. (The Daily Star, April 19, 2024).

Maoni:

Mratibu wa hafla hii, BIISS, ni taasisi ya kisheria na inazingatiwa kuwa mufakkir wa juu wa Bangladesh kwa masuala ya kimataifa, kiusalama na kimkakati. Wanajopo wengine kando ya Mkuu wa Jeshi ni pamoja na CGS (Mkuu wa Majenerali) Luteni Jenerali Waker-uz-Zaman, Makamu wa Jeshi la Wanahewa (Mstaafu) Mahmud Hussain, Meja Jenerali Mstaafu Ullah Chowdhury, Mkurugenzi Mkuu wa BIISS Abu Bakar Siddque Khan na Mwenyekiti wa BIISS aliyekuwa balozi AFM Gousal Azam Sarker. Matamshi ya Mkuu wa Jeshi na wengine katika mpango huu yanaakisi wazi utumwa wa kiakili wa jeshi na uongozi wa serikali katika kutafuta uhusiano wa kimataifa. Utumwa huu wa kiakili kwa makafiri wa Magharibi pia unafichua sababu ya kufeli kwa uongozi wa kisekula katika kulinda maslahi ya watu. Utumwa wa uongozi wa kijeshi sio tu ni fedheha wazi; ni hatari sana kwa Waislamu wa Bangladesh na ndicho kikwazo pekee kilichosalia ambacho kinauzuia Ummah mzima wa Kiislamu kusuluhisha mambo yake yote ya ndani na nje kwa njia ya haki na yenye athari.

Suala la kusawazisha kati ya dola kubwa mbili au zaidi zinazokinzana lilitokana na fahamu fisidifu ya ‘Mizani ya Nguvu za Jeshi’. Fahamu hii inaonyesha kwamba taifa lolote lililo na nguvu dhaifu za kijeshi lazima lisalie ndani ya mzunguko wa dola yoyote kuu ili kugeuza au kukabiliana na nguvu nyingine kubwa za kijeshi. Fahamu hii ni kichocheo cha tafakuri kwa mataifa ya Kiislamu na hii inahakikisha kwamba Waislamu daima watabaki chini ya utawala wa dola moja kubwa au nyingine, ambayo ina maslahi ya kikoloni. Nchi za Magharibi za kikoloni zinafundisha fahamu hii potovu ya kupagawisha watu kwa baadhi ya Waislamu ndani ya duru za uongozi wa Wanajeshi na Serikali na watu hawa waliopagawa na kufanywa watumwa na fikra hii ya 'ukuu wa Magharibi' wanaieneza hii kwa umma wa Kiislamu na kuwazuia Umma kutokana na kupambana na kubadilisha nafasi yake iliyohujumiwa na kushindwa. Lau kama fahamu hii iliwahi kuwa ya kweli na yenye ufanisi, basi kwa nini Waislamu waweke jeshi lao wenyewe? Je, ni uhalali gani wa kuwepo kwa maisha ya utumishi ya Jenerali Shafiuddin? Je, ‘nyota nne’ zilizopambwa kwa sare zake zina maana gani kwa watu wa Bangladesh? Ukweli ni kwamba uongozi wa kijeshi na serikali ya Bangladesh ni watumwa wa kiakili wa Magharibi katili na hawana haki yoyote ya kuwaongoza Waislamu nchini Bangladesh.

Ni ukweli wa kihistoria kwamba vizazi vya awali vya islamu vilikanyaga fikra ya ‘mizani ya nguvu za kijeshi’ chini ya miguu yao na kuunda Umma mtukufu wa Kiislamu kwa kuyashinda majeshi mengi yenye nguvu na fahari. Waislamu walianza na Vita vya Badr, kwa kufedhehesha jeshi la adui lenye idadi kubwa zaidi na nguvu. Kisha, kutoka al-Ahzab au Vita vya Handaki hadi Mutah, Yarmuk, na Qadisiyah, Waislamu kwa udhahiri walishinda jeshi moja lenye nguvu baada ya jengine; baadhi ya hayo yalikuwa dhidi ya dola kuu za zama hizo. Vizazi vya baadaye vya majeshi ya Kiislamu vilibeba urithi huo na kunyakua ushindi huko Ain-Jalut, Gaudalete (Uhispania), Aror (Sindh), na Nadia (Bengal) na kuendelea kubeba nuru ya Uislamu hadi Ulimwenguni kote. Kwa hivyo, katika historia yote, maneno 'mizani ya nguvu za kijeshi' haijawahi kuwepo katika kamusi ya Majeshi ya Waislamu, hadi hivi majuzi, ambapo, kwa kupatiliza fursa kubwa ya kukosekana kwa Khilafah, Makafiri wa Magharibi walishika hatamu za Majeshi ya Waislamu na kuanza kulemaza mabongo ya uongozi wa kijeshi na fikra hii takataka. Ushindi wa vizazi vya awali vya Waislamu dhidi ya majeshi makubwa zaidi ni ukweli usiopingika na haihitaji kitu cha kuthibitisha. Hata hivyo, tunapaswa kuelewa sababu ya matukio hayo mashuhuri ili kizazi cha sasa cha majeshi ya Waislamu kiweze kuiga na kurudia zama hizo za kishujaa sana hivi sasa.

‘Mizani ya Nguvu za Kijeshi’ ya ‘nadharia ya wanamamboleo’ inatokana na fahamu ya maslahi ya kimada. Ulimwengu wa kibepari ulihesabu biashara kati ya kujihusisha na vita na manufaa yanayohusiana na ukoloni, na kisha kuja na nadharia hii. Kwa hivyo, wanakadiria nguvu ya kimada ya majeshi yao kwa kushirikiana na maslahi yao ya kimada au manufaa (maslahi ya kikoloni) na kugundua kuwa haina maana kushiriki katika migogoro ya kijeshi isipokuwa ikiwa faida yakini na kubwa kuliko gharama. Hesabu hii ya ‘nguvu za kimada’ haina msingi wowote wa kimaadili, kwa sababu ilitokana na msingi wa fikra ya kikoloni; kwa hivyo nchi yoyote inayojilinda yenye jeshi dhaifu inaweza kushinda vita dhidi ya nguvu zaidi ya wavamizi/ukoloni ikiwa sababu ya maadili ya kutetea watu na mali imeamshwa. Kwa hivyo, nguvu ya maadili ya jeshi hutoa nguvu zaidi kuliko nguvu ya kimada ikiwa imeamshwa ipasavyo. Walakini, nguvu iliyo imara zaidi ni nguvu ya kiroho ya jeshi. Siri ya ushindi wa zamani wa Waislamu dhidi ya majeshi makubwa zaidi ni nguvu ya kiroho ya Waislamu. Majeshi ya Waislamu yalitoka nje kwa lengo la kiroho, sababu ya kueneza nuru ya Uislamu, sababu ya kutakasa ardhi kutokana na uchafu wa makafiri. Majeshi ya Waislamu yalisonga mbele kwa lengo la kueneza uadilifu wa Mwenyezi Mungu na yalikuwa na yakini kwamba Mwenyezi Mungu (swt) ataleta msaada wa Kiungu wakati wowote apendapo na kuwafanya Waislamu washinde. Majeshi ya Waislamu yalijiona kuwa ni ‘Naibu’ wa Mwenyezi Mungu Mtukufu katika uso wa dunia hii inayoondoka. Ukinaifu huu na mitazamo hii ilipelekea vizazi vya awali vya Waislamu kuwashinda maadui zao, ambao walitafuta tu manufaa ya kimada. Kwa hivyo, hiki ndicho kichocheo cha siri ambacho Majeshi ya sasa ya Waislamu yanapaswa kuiga. Ni wale tu maafisa wa kijeshi ambao wana lengo hili na ukinaifu huu wa kiroho katika nusra ya Mwenyezi Mungu ndio wanaopaswa kuongoza Majeshi ya Waislamu sasa; hapo ndipo Waislamu wataweza kusimamisha tena Khilafah yao na kutatua mambo yote ya ndani na nje. Ni hapo ndipo historia ya dhahabu itajirudia yenyewe na Ummah utakuwa na furaha baada ya karne iliyojaa huzuni na udhalilifu.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Risat Ahmed
Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir katika Wilayah Bangladesh

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu