Jumamosi, 25 Shawwal 1445 | 2024/05/04
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

Afisi ya Habari
Nchi Zinazozungumza Kijerumani

H.  2 Rajab 1445 Na: 1445 H / 02
M.  Jumapili, 14 Januari 2024

Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Serikali ya Shirikisho Inautoa Kafara Uaminifu wa Ujerumani
(Imetafsiriwa)

Baada ya mwaliko uliowasilishwa dhidi ya "Israel" kwa tuhma za mauaji ya halaiki kusomwa mbele ya Mahakama ya Kimataifa ya Haki jijini The Hague, Alhamisi, 11/01/2024, serikali ya Ujerumani ilitangaza kupitia afisi yake ya habari kwamba "mashtaka haya hayana mashiko na hayana msingi wowote.” Kwa kuongezea, serikali hii inakusudia kuingilia kati kama mhusika wa tatu katika kesi hiyo na kutetea umbile la Kiyahudi. Kwa mtazamo huu, serikali ya shirikisho inaidharau kabisa Ujerumani na kufichua maana kamili ya kile kinachoitwa maslahi ya kitaifa ya Ujerumani. Baada ya kuwajibisha watu wake “kuyatoa muhanga maisha yao ili kulinda usalama wa ‘Israeli’,” sasa inadhamiria kuzitoa kafara taasisi za mfumo wa kilimwengu kwenye makaburi ya Uzayuni.

Tangu kuasisiwa kwa umbile la Kiyahudi, Wazayuni wakuu wametangaza kwamba mauaji ya kimfumo na kuwafukuza watu wa nchi hiyo ni miongoni mwa misingi imara ya dola yao. Waziri mkuu wa kwanza wa umbile la Kizayuni, David Ben-Gurion, alizungumza kwa uwazi kuhusu "uvamizi, uharibifu na uhamisho," na alitaka kwamba "waliofukuzwa wasiruhusiwe kamwe kurudi." Aliendelea kusema: “Wazee watakufa na vijana watasahau.” Katika miongo iliyofuata, serikali zote za umbile hilo zilitumia kanuni hii. Rafael Eitan, Mkuu wa Majeshi wa Jeshi la Kizayuni, alisema mwaka 1983: “Tunatangaza waziwazi kwamba Waarabu hawana haki ya kukaa hata sentimita moja ya Eretz ‘Israel’...Nguvu ndiyo kitu wanachokifanya au watakachoweza kuelewa. Tutatumia nguvu ya mwisho hadi Wapalestina watakapokuja wakitambaa kwetu kwa miguu minne.”

Tangazo la vita la serikali ya Netanyahu mnamo Oktoba 7, 2023 linaangukia kabisa ndani ya sera hii ya kuangamiza na inawakilisha hadi leo hii kilele cha historia ya umwagaji damu ya Israel. Makumi ya maelfu ya Wapalestina wameuawa katika miezi ya hivi karibuni, wengi wao wakiwa wanawake na watoto, na asilimia thamanini ya Ukanda wa Gaza umeharibiwa kabisa. Takriban watu milioni mbili wameyakimbia makaazi yao kutokana na mashambulizi yaliyoenea, na zaidi ya watu milioni moja wanatishiwa na njaa kutokana na kuzuiliwa kwa utaratibu. Mashirika ya haki za binadamu ya Oxfam na Human Rights Watch yamethibitisha kwamba Wazayuni "wanatumia njaa kama silaha ya vita." Kwa kuongezea, kulingana na wataalam kutoka shirika la utafiti la Forensic Architecture, jeshi la Israel linaendesha kampeni ya kimpangilio dhidi ya miundombinu ya matibabu ya Gaza na, kulingana na Kamati ya NGO ya Kulinda Waandishi wa Habari (CPJ), "inalengwa kuua waandishi wa habari na familia zao.”

Vitendo vyote hivi vinalenga kusababisha hasara kubwa zaidi ya wanadamu na kuwaangamiza Waislamu huko Gaza. Haya yote yanawiana kabisa na kauli za serikali yenyewe ya Netanyahu. Huku waziri mkuu wa umbile la Kizayuni akifichua nia yake ya mauaji ya halaiki kwa kuregelea kuangamizwa kwa kabila la Amaleki katika Agano la Kale, rais wa umbile hilo, Isaac Herzog, alitangaza kwamba hakukuwa na watu wasio na hatia katika kampeni ya Gaza: "Ni taifa zima ambalo linawajibika. Maneno haya kuhusu raia kutojua, kutohusika, sio kweli kabisa. ... na tutapigana mpaka tuvunje uti wao wa mgongo.” Hata balozi wa umbile la Kizayuni jijini Berlin, Ron Prosor, alisema hadharani kwamba "ni makosa kutofautisha kati ya raia na Hamas."

Kauli hizi zitokazo kwenye midomo ya Wazayuni zinaifichua serikali ya Ujerumani na kufichua kuwa kauli yake iliyotangulia imefikia kilele cha ubaya na dharau! Badala ya kuzingatia kuwepo kwa tuhuma za awali za mauaji ya halaiki - na hii ndiyo kawaida katika mifumo ya kisasa ya kisheria - serikali ya shirikisho inatangaza mapema kutokuwa na hatia kwa watuhumiwa, ikisema: "Hata hivyo, serikali ya Ujerumani inakataa kwa hakika na kwa uwazi mashtaka ya mauaji ya halaiki yaliyoletwa dhidi ya Israel mbele ya Mahakama ya Kimataifa ya Haki... Shutuma hiyo haina msingi wowote.” Kwa kurejelea historia yake ya Wanazi, serikali ya Ujerumani inajaribu kudhibiti kile kinachoitwa Mkataba wa Mauaji ya Halaiki na kuutumia kwa malengo yake yenyewe, na kuuelezea kama "chombo kikuu [...] kuzuia kabisa kujirudia kwa kile kilichotokea katika enzi ya Nazi.”

Hili linathibitisha dhamira ya kisiasa nyuma ya ushirika na umbile la Kizayuni, na inadhihirisha hamu ya kuhalalisha hata mfumo wa kimataifa kwa madai ya sheria zake. Hivyo, Ujerumani inaungana na mhimili wa nchi hizo ambazo mienendo yao inadhihirisha hali halisi ya kile kinachoitwa sheria za kimataifa na taasisi za kimataifa, ikiwemo Mahakama ya Kimataifa ya Haki, ambayo ni nyenzo zilizo mikononi mwa dola za kikoloni, ambayo wanaitumia kwa mujibu wa maslahi yao!

Hizb ut Tahrir kwa mara nyingine tena inaikumbusha serikali ya Ujerumani kwamba ni lazima iwajibike kwa matendo yake, bila kujali hukumu ya Mahakama ya Kimataifa ya Haki. Iwapo inafikiri kwamba damu ya Waislamu si chochote ila ni kichocheo cha kujadiliana katika taratibu za mahakama zenye msukumo wa kisiasa, basi ifanye yafuatayo:

Khilafah ijao itabomoa kabisa mfumo wa kikoloni katika Mashariki ya Kati na itawawajibisha wale wote waliohusika na mauaji na kuyahama makaazi yao! Kushikamana na maslahi ya kitaifa yenye uharibifu ambayo yanaunganisha hatima ya kibinafsi na umbile la Kizayuni ni kosa la kihistoria, kosa ambalo Umma hautasahau kamwe, na pengine hata watu wa Ujerumani hawataisamehe serikali kwa kosa hili.

[وَقُلْ جَاءَ الْحَقُّ وَزَهَقَ الْبَاطِلُ إِنَّ الْبَاطِلَ كَانَ زَهُوقاً]

“Na sema: Kweli imefika, na uwongo umetoweka. Hakika uwongo lazima utoweke!” [Al-Isra:81]

Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir
 katika Nchi Zanazozungmza Kijerumani

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Nchi Zinazozungumza Kijerumani
Address & Website
Tel: 0043 699 81 61 86 53
Fax: 0043 1 90 74 0 91
E-Mail: shaker.assem@yahoo.com

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu